Timu ya TASA ikiwa pamoja na Wananchi wa Kata ya nalingu katika shughuli ya kijamii ya kuchimba msingi wa ujenzi wa Kituo cha Afya Nalingu. Hatua hii ni sehemu ya mikakati ya kuimarisha huduma za kijamii huku ikichochea umoja na mshikamano miongoni mwa wakazi wa eneo hilo.
Katika tukio hilo la kihistoria, TASA iliungana na Wanamabadiliko wa kata hiyo kupitia mradi wa Amani Yetu Kesho Yetu. Mradi huu unatekelezwa kwa ufadhili wa shirika la CEFA Tanzania kupitia programu ya Kujenga Amani Project inayofadhiliwa na Umoja wa Ulaya (European Union in Tanzania).
Ushiriki huu ulikuwa na lengo kuu la kuonyesha mshikamano na umoja wa vijana na wanawake katika kudumisha amani. TASA inaamini kuwa amani ya kweli inajengwa kupitia kazi za pamoja zinazogusa maisha ya watu moja kwa moja na kuchochea maendeleo ya jamii kwa haraka.
Kitendo cha kuchimba msingi wa kituo hiki cha afya ni kielelezo tosha kuwa amani na maendeleo ni vitu vinavyotegemeana. Kupitia nguvu za pamoja kati ya TASA, Wanamabadiliko, na wananchi wa Nalingu, jamii inaonyesha utayari wa kulinda amani ya kesho kwa kujenga miundombinu muhimu leo.
Tukio hili limeacha alama ya ushirikiano mkubwa na ni mwendelezo wa jitihada za TASA katika kuhakikisha vijana wanakuwa mstari wa mbele kwenye harakati za amani na maendeleo nchini Tanzania.


